RT ILIVYOISUKA UPYA KATIBA YAO.....

Posted in
No comments
Tuesday, August 6, 2013 By danielmjema.blogspot.com



Na Athumani Issa, Moshi

VYAMA vingi vimekuwa vikijikuta vikiingia katika Migogoro ya mara kwa mara kutokana na kukosa miongozi sahihi ya kuhakikisha matatizo yote yanayojitokeza yanatatuliwa kisheria.
Moja ya Vyombo muhimu vinavyoweza kutumika kutatua migogoro hii hasa ukizingatie penye watu wengi lazima kuwe na migongano ya kimawazo kama sio kimaslahi.

Katika kutambua hili shirikirisho la Riadha Tanzania (RT),katika  mkutano wake mkuu uliofanyika Julai 27 na 28 mwaka huu, mjini  Morogoro, imeazimia kuhakikisha hali kama hii haijitokezi kabisa na kama imewahi kujitokeza basi isijirudie tena.

Katika kuhakikisha hilo, RT chini ya Rais wake, Anthony Mtaka ilitangaza kuingia katika mchakato wa kuandaa katiba ambapo ilimteua Mwanasheria wake, Thabit Bashiri kusimamia mchakato huo ambaye katika mkutano mkuu uliofanyika Mjini Morogoro aliwasilisha Rasimu ya Katiba kwa wajumbe wa Mkutano.

Hivyo basi ili kuhakikisha umma unapata kuelewa kilichomo ndani ya Rasimu hiyo, Taifa Letu.com ilimtafuta Thabit Bashiri na kufanya naye mahojiano ya kina ambapo alizungumza mambo kadha wa kadha ikiwemo baadhi ya mambo muhimu aliyoyazingatia katika kuunda Rasimu hiyo ya
Katiba.

Bashiri anazungumzia mambo mbali mbali ambayo kutokana na uzoefu wake na Taaluma yake anaamini kama yatazingatiwa na kama yangezingatiwa na Vyama vingi vya Michezo Tanzania na Duniani kote kwa ujumla, migogoro yasiyokuwa na lazima yasingetokea, na hapa anaelezea moja baada ya nyingine:

Taifa letu.com: baada ya kupewa kazi ya kutengeneza Rasimu ya Katiba ya Shirikisho la Riadha Taifa, ni changamoto gani uliziangalia?
Mwanasheria: Ukweli ni kuwa nilifahamu kuwa moja kati ya matatizo makubwa yanayovikumba vyama vya michezo nchini Tanzania na barani Afrika kwa ujumla ni ubovu wa katiba zao.
Ubovu wa katiba kwa asilimia kubwa ndiyo unachangia matatizo mbalimbali katika vyama vyetu kama  kutokuwa na vyanzo vya mapato vya kutosha, migogoro isiyoisha, rushwa, uchaguzi usio na haki, ufujaji wa mali za chama, unyanyasaji wa kijinsia, ugandamizwaji kwa wachezaji,
maamuzi yasiyo na haki n.k . Hivyo basi moja kati ya malengo yangu makuu ilikuwa ni kuja na rasimu ya katiba ambayo itakuwa na lengo la kuwa suluhisho la matatizo hayo.

Taifa letu.com: Katiba ya zamani haikuwa na yapi ambayo kwa sasa umejaribukuyazingatia?
Mwanasheria: Katiba iliyopita haikuwa na utambuzi kwa wadau mbalimbali  wa Riadha kama Klabu za Riadha, wawakilishi wa wachezaji,wahamasishaji (Promoters) na hivyo kusababisha sio tu kukosa mapato bali pia kukosa nguvu ya kuendeleza riadha nchini Tanzania.
Pia katiba iliyopita ilikuwa na utaratibu uliopitwa na wakati wa utatuti wa migogoro kiasi kwamba ilishindwa kudhibiti na kuamua migogoro mbalimbali kwa usawa.

Lakini pia iliruhusu matumizi holela ya fedha za chama,hapakuwa na udhibiti mzuri wa fedha za chama hivyo kusababisha chama kukosa uaminifu mbele ya jamii na hivyo wadau na wadhamini kukikimbia na kukifanya kuwa masikini. Hivyo wakati wa kutengeneza rasimu hii mpya, mambo hayo yote nimeyazingatia katika kurudisha imani kwa wananchi na wadau wa riadha ndani na nje ya nchi.

Taifa Letu.com
: Je Katiba hii itakuwa na msaada gani kwa RT na Watanzania wapenda Riadha kwa ujumla?

Mwanasheria: Rasimu hii imelenga katika kuifufua Riadha upya kuanzia vijijini mpaka mijini, kuleta mahusiano mazuri baina ya wadau wa Riadha na kuleta uwiano wa kijinsia katika ushiriki na uongozi wa Riadha.Rasimu hii inalengo la kumfanya mwanariadha au kiongozi ajivunie kuwa ndani ya familia ya Riadha na aweze kushiriki kwa dhumuni la kuitangaza na kuiendeleza Riadha Tanzania.
Kwanza, nilipata fursa ya kujionea maendeleo ya vyama vya Riadha katika nchi zilizopiga hatua katika mchezo wa Riadha, kwa mfano Nchi kama Kenya, Afrika ya kusini, Msumbiji, Ghana na Zambia zimeweza kuwa na Katiba bora ambazo zimekuwa chachu ya maendeleo ya Riadha hasa
katika kuwavutia wadhamini.

Sio hivyo tu, ubora wa Katiba zinazoendesha vyama vya nchi hizo nilizozitoea mfano umechangia kikubwa  kuongezeka kwa vyanzo vya mapato, kuungwa mkono na wadau mbalimbali, uratibu mzuri wa migogoro na uimarishaji thabiti wa viwanja vya michezo hasa katika mchezo huu
wa Riadha.

Taifa letu.com: Lakini Mwanasheria, bado sijaona ni kwa namna gani Rasimu hii ya ilivyoweza kuzingatia uhamasishaji wa ushiriki wa wanariadha wa kike ukizingatia kuwa kumekuwa na uhaba wa wanariadha wa kike wanaoshiriki au kuwania uongozi katika nyadhifa mbalimbali ndani
ya Mchezo huu?
Mwanasheria: Katika mambo ambayo nimeyaingiza kwa makusudi ni kuweka vifungu ambavyo vinailazimisha kamati ya utendaji kuteua wanawake wawili kwa kila kamati ndogo watakazoteua.
Lengo kubwa ni kukuza uhamasishaji katika mchezo huu ambapo kadri siku zinavyozidi kwenda ushiriki wa wasichana unazidi kupungua na hivyo kuwakosesha wasichana kupata fursa ya kufaidika kutokana na vipaji vyao na sio hilo tu pia katika rasimu hii nimejaribu kuangalia umihimu wa kuingiza suala la kamati ya wanawake ambayo kwa asilimia kubwa itawakilisha sauti ya wanawake katika familia ya Riadha

Taifa Letu.com: Kumekuwa na matukio ya matumizi ya Madawa ya kuongeza Nguvu miongoni mwa wanariadha, mfano hivi karibuni tulisikia sakata la mwanariadha wa Marekani,Tyson Gay, kukutwa na kosa la kutuia madawa ya kulevya, rasimu hii imejiandaa vipi kukabiliana na hilo?
Mwanasheria: Moja kati ya mambo muhimu ambayo yanahitajika kuwa katika katiba yoyote ya chama cha Riadha ni kuwa na katiba ambayo inaunga mkono upingaji wa madawa ya kulevya unaofanywa na WADA (World Anti-Doping Agency).
Hivyo rasimu hii moja kwa moja inaunga mkono uchunguzi wa wachezaji kuhusu matumizi ya madawa ya kuongeza nguvu ambao utakuwa ukifanywa kila kwenye mashindano yanayoandaliwa na RT na kutuma taarifa kwenda kwenye Shirikisho la Riadha Duniani.

Taifa Letu.com: Kumekuwa na matukio ya matumizi mabaya ya Fedha ambayo uzoefu unaonesha kuwa ndio chanzo kikuu cha migogoro ndani ya vyama vingi vya michezo, hili nalo limezingatiwa vipi katika rasimu hii au ndio mradi mambo yaende?
Mwanasheria: Kwanza nikushukuru Ndugu mwanadishi kwa Swali lako zuri, katika Rasimu hii nimeweza kuainisha vyanzo mbalimbali vya mapato ambavyo RT inaweza kuvitumia na kunufaika navyo na hivyo kuwa na fedha ya kuweza kusimamia shughuli zake ikiwemo kulipa wafanyakazi,
kusafirisha timu ndani na nje na kuandaa mashindano.

Pia rasimu hii imeweza kuainisha njia nzuri za matumizi ya fedha zipatikanazo kutokana na vyanzo mbalimbali, ambapo imeelezwa wazi kuwa fedha yoyote ipatikanayo katika RT ni kwa madhumuni ya kuendeleza mchezo wa Riadha, hivyo kutakuwa na uwasilishwaji na upitishwaji wa
taarifa za fedha kwa kamati ya fedha, kamati ya utendaji na kwenye mkutano mkuu.

Nafahamu swala la uaminifu nalo ni tatizo miongoni mwa baadhi ya viongozi wetu, ukisoma kwa makini rasimu hii utagundua kwamba hili nalo halijaachwa, imeanishwa vizuri katika rasimu kuwa kutakuwa na mkaguzi huru wa mahesabu atakayekagua taarifa zote za fedha za chama huku vyama vya mikoa vikihitajika pia kuwasilisha taarifa zao za fedha kila mwaka, lengo ni kuhakikisha fedha zinatumika kwa dhumuni moja tu la kuendeleza mchezo wa Riadha nchini Tanzania.

Taifa Letu.com: Mwanasheria utakubaliana na mimi kuwa utatuzi wa migogoro ndani ya Vyama vingi vya michezo umekuwa wenye mashaka na mara nyingi kumekuwa na malalamiko kuhusiana na swala hili, vipi Rasimu hii inashughulikiaje hilo tatizo?
Mwanasheria: Bila shaka Ndugu mwandishi, hilo liko wazi kabisa, tunafahamu kuwa katika vyama vya michezo, migogoro ndiyo tatizo kuu ambalo hudumaza michezo na maendeleo ya vyama, hii inatokana na utaratibu mbovu na wa kiuonevu na usiotoa haki kwa aliyekosa au aliyekosea na hivyo kusababisha migogoro kuendelea kila kukicha na kudumaza michezo.
Rasimu hii imeanzisha kamati tatu za sheria, Kamati ya Maadili, Kamati ya Nidhamu na Kamati ya Rufaa katika kutatua makosa mbalimbali ya kinidhamu ya chama na wanachama wake.

Pia Katiba imeanzisha baraza la usuluhishi kwa ajili ya kutatua shauri lolote kati ya wanachana na chama, mchezaji na chama au mchezaji na mchezaji. Katiba imeweka wazi umuhimu wa kutambua mahakama ya usuluhishi wa Michezo (CAS) iliyopo Lausanne, Switzerland hivyohaitaruhusiwa  kwa shauri la kimichezo kupelekwa katika mahakama zisizo za kimichezo.

Taifa Letu.com: Ahsante, kuna lipi jipya ambalo rasimu hii imeongeza ili kuleta chachu ya Maendeleo ya Riadha nchini na pengine kuturudisha katika enzi za mafanikio ya akina Filbert Bayi na Suleiman Nyambui?
Mwanasheria: Mengi sana, tumejaribu kupendekeza mashindano mapya baina ya mikoa na mikoa (Inter-regional), pia mashindano ya taifa ya klabu za Riadha na mashindano ya mikoa ya klabu za Riadha.
Pamoja na hayo, taasisi za elimu na majeshi zimepewa uanachama shirikishi, lengo hapa ni kuchochea uhamasishaji wa mchezo huu kuanzia vijijini mpaka mijini na pia kutoa wigo mpana wa kupata wachezaji wengi kwa kadri inavyowezekana.

Pia katiba hii imediriki kuimarisha uhusiano baina ya RT na vyama vya mikoa vya Riadha, hii inatokana na kudorora kwa mchezo huu mikoani hivyo kuhitajika juhudi za dhati katika kuhakikisha kuwa vyama vya mikoani vinaamka na kufanya kazi iliyokusudiwa kwa maendeleo ya
wanariadha na watanzania kwa ujumla.

Taifa Letu.com: Wadau na Wanachama wanatawezaje kutoa mchango wao kwenye rasimu hii?
Mwanasheria: Baada ya kupita katika kamati ya utendaji na kufanyiwa marekebisho kadhaa, rasimu hii itatumwa kwa wanachama na wadau wote Tanzania nzima na watahitajika kutoa maoni yao kuhusu rasimu ya katiba hii kabla ya kuipitisha katika mkutano mkuu ili kuanza kutumika rasmi.
Taifa Letu.com: Nakushukuru sana Mwanasheria, ila kabla hatujaagana ushauri wako kwa wadau wa riadha kwa jumla ni nini?
Mwanasheria: Binafsi ningependa kuwaomba kwa dhati, kuipitia rasimu hii ya katiba kwa ajili ya maendeleo ya mchezo huu Tanzania, Naamini Riadha ndiyo mchezo pekee ambao kama tukiutolea mkazo tunaweza kupeperusha bendera yetu katika ushiriki wa ngazi za kimataifa.
Tanzania imejaaliwa kuwa na wanaridha wa aina zote,wanariadha wa mbio ndefu na fupi,miruko na hata mitupo,hivyo kama tutatumia vizuri fursa hii,tunaweza kuwa na katiba bora ambayo itaweza kuleta maendeleo ya riadha nchini Tanzania,kupunguza tatizo la ajira na kusaidia ujenzi wa
taifa kupitia mchezo wa Riadha.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Riadha yetu!!

0756038214/0654724337



www.kijiwechetu.blogspot.com

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .