MAANDALIZI YANAHITAJIKA MBIO ZA 'SOKOINE DAY'

No comments
Monday, April 14, 2014 By danielmjema.blogspot.com

SOKOINE Min Marathon 2014 imefanyika mwishoni mwa wiki kuadhimisha miaka 30 ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Edward Moringe Sokoine, kijijini kwake Monduli Juu mkoani Arusha.

Waziri huyo alitajwa na Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, kwamba alikuwa mwerevu sana, licha ya kwamba Mwalimu alisema werevu kila mmoja anao hata shetani naye ni mwerevu sana, kubwa zaidi kwa Edward lilikuwa ni hodari wa kazi.

Hii ndio sababu hata Taifa linakumbuka kuadhimisha kutokana na ukweli kwamba alikuwa na uwezo wa kufanya kazi siku mbili hata tatu bila kulala hii ilitokana na wema wake na upole kwa watu wa taifa la Tanzania.

Rais Jakaya Kikwete kwa mara ya kwanza tangu aingie madarakani, alikuwa mgeni rasmi wa Kumbukumbu ya Kifo cha Sokoine, ambako alihutubia umati wa watu uliofurika katika kaburi la kiongozi huyo shupavu aliyeacha historia kwa Tanzania na kuweka shada la maua juu ya kaburi hilo.

Siku hiyo ilifana kutokana na uwepo kwa michezo mbalimbali ikiwemo riadha, miruko, kurusha mikuki nk, ambapo wanariadha nguli walipambana vilivyo katika ‘Sokoine Day 2014.’

Nilichojifunza katika  sherehe hizo, mchezo wa riadha unakua kwa kasi nchini hivyo ni vema ukapewa kipaumbele kutokana na ukweli kwamba una historia nzuri hapa nchini ambayo bila juhudi tutabakia katika makabrasha ya historia, kwamba miaka ya 1960 hadi 1990 ulikuwa juu.

Wanariadha wa kujitegemea kina Fabian Joseph (Arusha), Nathalia Elisante (Arusha) Mary Naali, Selina Amosi (Zanzibar) walikimbia mbio za kilometa 10 na kutoa ushindani wa hali ya juu.

Holili Youth Athletics Club (HYAC) haikuwa nyuma, nayo iliweza kufurukuta na kuibuka washindi chipukizi katika kilometa 2 wasichana, ambako Adelina Audax aliwaongoza wasichana wenzake akifuatiwa na Neema Mathias na nafasi ya tatu kunyakuliwa na Lidiuna Godfrey wote kutoka klabuni hapo.
Sakilu akimaliza mbio
Wanafunzi wa Shule za Msingi na Sekondari kutoka maeneo ya karibu na Monduli Juu walishiriki na kutoa ushindani wa juu kuwahi kushuhudiwa, kutokana na wanafunzi hao kunirudisha miaka ya nyuma wakati Umitashumta na Umiseta  ulipokuwa ukifanya vema katika kuibua vipaji vya riadha.

Kubwa zaidi mbio hizo ziliathiriwa na msafara wa viongozi wengi wa kisiasa waliokuwa wakimiminika kwa ajili ya maadhimisho hayo muhimu nchini Tanzania, kwani mbio zilipokuwa zikianza wanariadha walijikuta wakisongamana eneo moja hali iliyosababisha wasikimbie kwa muda mzuri.
Alphonce Felix akimaliza mbio hizo katika nafasi ya pili baada ya Fabian Joseph
 Katika mbio kinachoangaliwa ni muda ambao mwanariadha anakimbia kwani amekuwa wa kwanza ama wa mwisho ni kitu kingine ambacho kwa wanaotafuta vipaji vya wanariadha watakachoangalia ni muda aliokimbia mwanariadha husika.

Mshindi wa Kilometa 10 katika kuadhimisha miaka 30 ya kifo cha Sokoine, Fabian Joseph alikimbia kwa dakika 34:28.04 huku Alphonce Felix (Holili Youth Athletics Club) alikimbia kwa dakika 34:45.39 na Dickson Marwa (Holili Youth Athletics Club) bingwa wa mbio hizo mwaka 2013 alikimbia kwa dakika 34:57.47.
Mgeni Rasmi wa maadhimisho ya mwaka huu, Rais Kikwete akiwa na wake wa Sokoine pamoja na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa
Kitaalamu ukiangalia muda waliokimbia wanariadha hawa hauridhishi kabisa, kwani Alphonce Felix (HYAC) Bingwa wa Mbio za Mwaka Mpya 2014 zilizofanyika Jijini Dar es Salaam kwa umbali huo huo alikimbia kwa dakika 28:11.35, ukiangalia sababu ya kushuka ni kutokana na utiriri wa magari ya waheshimiwa, ukiwamo pia ubovu wa barabara uliojaa tope.

Gidabuday-mratibu wa mbio
Nilicheka kidogo wakati nilipoona kwa macho yangu ‘kijiko’ cha TANROADS kikichonga barabara asubuhi wakati wanariadha walipokuwa wakikimbia na kwa bahati mbaya sana mvua ya manyunyu ikiwa imelifunika anga na kijiko hicho kikakataa kurudi nyuma na kuziba barabara.

Wanariadha waliokuwa wajanja ndio waliovuka hapo wengine walikata tamaa kabisa ya kuchukua taji, najua wazi kuwa barabara ilikuwa ikiwekwa kifusi ili waheshimiwa viongozi wasikwame.

Ili tusikwamishe riadha nchini, ni vema ikafanyika siku moja kabla ya tukio la Kumbukumbu ya Sokoine, ili na watu wa eneo lile waweze kujipatia kipato kutokana na uwepo wa watu wengi ndani ya siku tatu au nne hivi.

SOURCE:Tanzania Daima

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .