UCHAGUZI TOC NI FURSA YA KUDEKI “MATAPISHI” YA OLIMPIKI 2012

Posted in
No comments
Thursday, November 15, 2012 By danielmjema.blogspot.com


Kama ulimiss makala haya yaliyochipishwa katika Gazeti lako pendwa la MTANZANIA la Tarehe 26 Octoba mwaka huu. yasome hapa na uweze kupata uelewa wa muelekeo wetu katika michezo!!

Na Fadhili Athumani, Moshi

Mitaani huwa kuna msemo usemao ukiona vyaelea ujue vimeundwa, msemo huu umejizolea umaarufu hasahasa pale ambapo kuna jambo nzuri limetokea na nadra kukuta linatumika panapootokea matatazo au mapungufu yoyote yale katika jamii

Naamini kila mwanamichezo anafahamu kwamba mwaka huu 2012 ni mwaka wa uchaguzi na bila ajizi vyama vyote vinavyosimamia maswala ya michezo hapa nchini kwa kuzingatia katiba zao vimekuwa katika hekaheka za kuhakikisha kuwa wanatumia vema fursa hii ya kuwaadhibu baadhi ya viongozi wao katika uongozi unaomaliza muda wao au kuwapongeza wacha[pa kazi kwa kuwachagua tena kuendelea kuwatumikia

Baada ya TFF kupanga kufanya uchaguzi Desemba hii, TAFCA wakitazamia kufanya ya kwao Novemba 25 huku vyma vya mikoani nazo zikihakikisha zinafanya chaguzi zao mapema kupisha chaguzi za kitaifa, kamati ya Olimpiki nchini (TOC) nayo imetangaza tarehe ya uchaguzi wa viongozi wake taifa baada ya viongozi walioko madarakani kumaliza muda wao, uchguzi ambao kwa mujibu wa katibu mkuu anayemaliza muda wake, Filbert Bayi, utafanyika Desemba 8 mwaka huu, mkoani Dodoma

BAADHI YA WASHIRIKI WA OLIMPIKI-LONDON 2012
Tayari Mwenyekiti wa sasa wa TOC, Gulam Rashid na Katibu Mkuu wake, Filbert Bayi wameshaonesha dalili zote za kutaka kutetea nyadhifa zao kitu ambacho kwa mujibu wa katiba ya TOC sio dhambi kwani, kikakatiba wanahaki ya kufanya hivyo kutokana na katiba ya ToC kubainisha wazi kwamba hakuna ukomo wa Kuongoza kamati hiyo nyeti inayosimamia mashindano ya Olimpiki, sekta nyeti na muhimu sana katika michezo kutokana na kuhusika moja kwa moja kukuza na kuibua vipaji vya michezo hususan Riadha

 Naomba niweke wazi mapema kwamba mimi binafsi yangu sina tatizo na nia ya waheshimiwa hawa kugombea tena kuongoza TOC katika maswala mazima ya kuendesha michezo na kusimamia program za kamati hiyo hapa nchini lakini naomba niwakumbushe tu kuwa “ukiona pana fuka moshi ujue pana moto hata kama ni kijinga” na kuwakumbusha kwa nia njema tu wasisahau kazi iliyoko mbele yao ya kudeki matapishi ya wawakilishi wetu katika mashindano ya Olimpiki 2012 yaliyomalizika hivi karibuni jijini London.

Katika uchaguzi wa Desemba ambao naamini lengo lake ni kurekebisha makosa tuliyoyafanya hapo nyuma, kamati ya TOC inayomaliza muda wake chini ya Mwenyekiti Gulam Rashid imeshabainisha majina ya wajumbe wanne wa kamisheni itakaosimamia uchaguzi na kuhakikisha kwamba kile kilichodhamiriwa kinatimia kwa kutupa viongozi makini kwa kufanya uchaguzi wa huru na haki, itafanya kazi yake na naamini kuwa timu hiyo ya Harrison Chauro, Hamis Ally Mzee, Abdalla Juma na aliyekuwa mwenyekiti wa timu ya Yanga, Loyd Nchunga haitafanya makosa

Kila la kheri kwa wagombea wote wa nafasi ya Uenyekiti, Makamu mwenyekiti, Katibu mkuu, Katibu msaidizi, Mwekahazina, Mweka Hazina msaidizi na wajumbe kumi wa mkutano mkuu, watano kutoka Bara na watano wengine kutoka Visiwani, nawatakia kila la kheri mara nyingine katika azma yenu ya dhati ya kutaka kuleta mageuzi ndani ya TOC na ikiwezekana kuhakikisha katika mashindano yajayo ya Olimpiki aibu tuliyoipata katika mashindano ya mwaka huu haijirudii tena ambapo washirki wetu waliishia tu kuwa watalii!

Namjua wengi watashangaa kwa nini nimesisitizia kuwapongeza wagombea waliojitokeza kuwania nafasi mbalimbali ndani ya TOC nakuwatakia kila la Kheri katika uchaguzi huo wa Desemba, sifanyi kwa sababu ya kuwapigia kampeni, la hasha, natumia fursa yangu kama mwanamichezo kuwa kumbusha watanzania wote wenye uchungu na nchi yao pamoja na viongozi ndani ya TOC kuhusu umuhimu wa kuweka matakwa ya Taifa mbele kwanza halafu yafuate matakwa yetu binafsi na hili naomba wagombea wote ndani ya TOC walitilie maanani

Nakumbuka baada ya Kenya kufanya vibaya katika Olimpiki ya mwaka huu kwa kujinyakulia medali kumi na moja tu katika michezo yote waliyoshiriki, wanamichezo wan chi hiyo wakiongozwa na serikali ya Rais Kibaki, walichukizwa na matokeo hayo manbaya kuwahi kutokea katika historia ya Kenya katika mashindano hayo na mengine mengi ya  kimataifa, kiasi cha kuamua kuunda Tume ya kuchunguza  sababu za wanamichezo wake kufanya vibaya

Nakumbuka katika Hotuba yake, mara baada ya Timu hiyo kurejea Nyumbani, Rais Kibaki alisikika akisema kuwa kitendo cha nchi yake kufanya vibaya katika Mashindano ya Olimpiki ambayo yeye kwa mtazamo wake ilikuwa ni fursa ya kuitangaza nchi ya Kenya, ni tusi kubwa kwa Uhuru wa Nchi hiyo, ni tusi kwa Wananchi walipa kodi wa Nchi hiyo, kutokana na Fedha zao kutumika katika Kugharamia Safari ya Wanamichezo hao

Rais Kibaki anasema, ni aibu kwa nchi yenye Rasilimali zote kupata matokeo mabaya kama hayo, huku akiishukia kamati ya Olimpiki ya nchi hiyo iliyoko chini ya Uenyekiti wa mwanariadha Mkongwe, Kipchoge Keino, pamoja na Wizara yenye Dhamana ya Michezo na kuwalaumu kwa kuchangia kufanya vibaya kwa nchi ya Kenya katika Michezo hiyo kwa kushindwa kuandaa kikosi imara nay a kiushindani

Sio Kibaki tu, kwani hata Wasanii wa Nchi hiyo ambao ni kio cha Jamii, hawakuachwa nyuma katika kukosoa, kuzungumza na kukemea yale ambayo wao waliona wanafaa kuyakemea kama wawakilishi wa wengi kutokana na kufanya vibaya kwa kikosi cha Olimpiki na mmoja wao ni msanii, Hubert Nakitare maarufu, Nonini , aliyesikika waziwazi akiikosoa kamati ya Olimpiki ya Kenya (NOCK) kwa kuchangia kufanya kwao Vibaya katika michezo hiyo kwa kuendekeza migogoro isiyokuwa na lazima

Wakati Rais Kibaki na Msanii Nonini wakijitokeza kuishtumu, cham,a cha Riadha ya Kenya(AK),na Kamati ya Olimpiki nchini mwao, cha kushangaza na kusikisha ni kwamba pamoja na Tanzania kufanya utumbo katika michezo ya London, hakuna na kiongozi hata mmoja, sio Rais, Waziri wala Msanii yeyote aliyejitokeza kuzungumza aibu tuliyoipata katika michezo ile na cha kusikitisha zaidi ni kuona viongozi wetu wa sasa ndani ya TOC wakitokea matamko yakuhuzunisha na kukatisha Tamaa kwa kusema kuwa hata kule kushiriki tu ni sifa kwa nchi, kweli?

Kuna mtu mmoja ambaye mwanzoni kutokana na kauli zake mimi binafsi nilikuwa namuona kama kachanganyikiwa, naomba nitumie makala haya kumtaka radhi ndugu yangu, mwanariadha maarufu nchini, aliyeliletea taifa heshima katika enzi zake na nathubutu kusema bila woga wowote kuwa, Wilhelm Gidabudayi,  ni mwanamichezo wa kweli na mfano wa kuigwa kutokana na kujitolea kwake kuzungumza na kukemea yale ambayo yeye kwa upeo wake aliona yanafaa kuzungumzwa ili watanzania waweze kufahamu uozo ulioko ndani ya  TOC

Gidabudayi katika kutetea kauli zake aliwahi kuhoji maandalizi na uteuzi wa kikosi kilichotuwakilisha katika michezo ya Olimpiki kwa kusema kwamba kudai kwamba kikosi hicho hakikuwa tayari kushiriki mashindano hayo na nakumbuka Gidabudayi alifikia mahali na kudai kikosi kutwa medali yoyote katika michuano hiyo ilikuwa ni ndoto, akitishia hadi kuchoma vyeti vyake vyote endapo Tanzania ingerudi na medali hata moja katika michuano, mwanzoni nilimwona Gidabudayi kama mchochezi na msaliti asiyefaa katika jamii, lakini ‘Mungu sio Athumani’, maneno ya Gidabudayi hata hayajakauka nadhani kila anelewa kilichofuata?!

Nakumbuka na nikimnuku Gidabudayi aliwahi kusikika akisema,” TOC ya sasa imeoza na kama kweli Watanzania wana hamu ya kufanya vizuri kwenye michuano ijayo ya Olimpiki ni lazima kitu kifanyike kwenye ile kamati tofauti na hapo ni kutwanga maji kwenye kinu, nashauri Wizara ya michezo ishtuke kwa nini TOC inasema haihusiki? Maana kama wadau wakubwa na viongozi wa michezo hapa nchini, TOC iende eneo la tukio(mashinani kutafuta washiriki wa Olimpiki 2012), kuliko kukaa kusubiri iletewe wanamichezo ndipo iwaandae,"
 Mwandishi wa Tanzania Daima, Irene Mark akimkaribisha katika Chumba cha Habari Katibu wa Hanang Sports Club, Wilhelm Gidabuday walipotembelea ofisi za gazeti hilo leo.

Sasa kinachonipa wazimu zaidi ni ile kauli ya TOC kupitia Katibu wake, Filbert Bayi kuwa TOC kama kamati ya Olimpiki nchini haiusiki katika maandalizi ya timu na kuongeza kuwa maandalizi ya kikosi ya timu zinazoenda katika Olimpiki kuanzia katika uteuzi wa wanamichezo ni kazi ya Chama cha Riadha (RT) kwa kushirikiana na vyama vingine na kkwamba kazi ya TOC ni kuratibu safari ya kikosi! Hapa Napata kichefuchefu kutokana kupata maswali mengi yasiyokuwa na maji kwamba kama TOC haihusiki na shughuli hizo walizozitaja wao Basi kazi yao hasa ni nini? na kama hawahusiki na maandalizi ya Kikosi hicho nyeti kuna umuhimu gani ya wao kuwepo? Hapa kwa kweli naomba maelekezo

Ni matumaini yangu kwamba wakati tunaingia katika uchaguzi mkuu wa TOC, mwezi Desemba mwaka huu, tutakumbuka umuhimu wa uchaguzi huo katika kubadli mwelekeo wa michezo hapa nchini na kurudia enzi za nyuma ambapo Taifa, iliweza kutoa wanamichezo wazuri kama, Wilhelm Gidabudayi, Filbert Bayi na wengine wengi ambao naamini nikianza kuwataja hapa tutakesha ambao kwa kujituma walithubutu kutoa upinzani kwa wanaridha nguli kama Kipchoge Keino na wengineo

Naamini kama kutakuwa na mikakati mizuri katika uongozi wa michezo kwa kuanzia kuingiza watu makini ndani ya TOC, kile kilichotokea katika michezo ya juzi ya Olimpiki, mashindano ya Riadha ya Kilimanjaro Marathon msimu wa 12, yaliyoshuhudia nchi jirani ya Kenya wakiondoka na medali yote mbele ya macho yetu na katika Ardhi yetu, hakitajirudia tena!

Mwisho kabisa niwatakie kila la kheri wagombea wote wa nafasi mbalimbli ya uongozi ndani ya kamati ya Olimpiki (TOC), nikitegemea kwamba ujio wao utakuwa ni mwanga na mwanzo mpya hapa nchini, tukumbuke kwamba, Wilhelm Gidabudayi, Filbert Bayi, Gulam Rashid na yeyote Yule ambaye anajitambua kama mwanamichezo, sote kwa pamoja kazi yetu ni kujenga nyumba moja; Tanzania. Na naamini kwa hayo nimewasilisha hoja ya Michezo ni Afya na Ajira.Mungu ibariki Tanzania!

0756038214/0654724337

MWISHO 

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .