MPAKISTANI WA UTOROSHAJI TWIGA AONEKANA AKIJIVINJARI MITAANI HUKU JESHI LA POLISI LIKIHAHA KUMSAKA KILA KONA

Posted in
No comments
Friday, May 2, 2014 By danielmjema.blogspot.com

Na Mwandishi Wetu, Moshi 
 
Raia wa Pakistan, Kamran Ahmed anayetafutwa kwa udi na uvumba na vyombo vya dola nchini, anadaiwa kuonekana akirandaranda katika mitaa mbalimbali ya mji wa Moshi.
Raia huyo wa Pakistan anatafutwa kufuatia amri ya kukamatwa kwake iliyotolewa na mahakama Machi 24 mwaka huu baada ya mtuhumiwa huyo kutofika mahakamani bila taarifa yoyote.
Mshitakiwa huyo pamoja na watanzania watatu, wanakabiliwa na mashitaka ya kusafirisha kinyume cha sheria, Wanyamapori hai 152 wakiwamo Twiga wanne, kwenda Jiji la Doha nchini Qatar.
Twiga hao na wanyama wengine wenye thamani ya Sh170.5 milioni, walitoroshwa kwenda Uarabuni Novemba 26,2010 kupitia uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (Kia).
Wanyama waliotoroshwa kwenda Doha wenye thamani ya Dola 113,715 za Marekani sawa na Sh170.5 milioni za Tanzania, walisafirishwa kwa kutumia ndege kubwa ya Jeshi la nchi ya Qatar.
Habari zilizopatikana jana zilieleza kuwa pamoja na mtuhumiwa huyo kusakwa kwa udi na uvumba, lakini Jumamosi iliyopita saa 6:00 mchana na juzi saa 2:20 usiku, alionekana katika mitaa ya Moshi.
Kwa mujibu wa mtoa habari wetu, Jumamosi alionekana akiwa katika gari aina ya Toyota Noah katika barabara ya J.K Nyerere na juzi alionekana akitoka kununua mahitaji Rafiki Supermarket.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz alipoulizwa jana, alisema wanazo taarifa za kutafutwa kwake kutokana na amri hiyo ya mahakama lakini bado hawajafanikiwa kumpata.
“Tuna habari na jambo hilo (kutafutwa) bado tunamtafuta,”alisema Boaz na alipoelezwa juu ya kuonekana kwake, alishtushwa na taarifa hizo na kuwataka wenye taarifa sahihi kumpatia.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mkoa wa Kilimanjaro, Simon Kobelo anayesikiliza kesi hiyo alipoulizwa jana, alisema amri ya mahakama iko pale pale na wenye wajibu wa kumtafuta ni polisi na wadhamini wake.
Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa kwa siku mbili, Mei 6 na 7 mwaka huu na mahakama imeshatoa ilani ya kuwaita wadhamini wake siku hiyo ili wajieleze kwanini wasichukuliwe hatua za kisheria.
Mbali na kesi hiyo, lakini mshitakiwa Ahmed anakabiliwa na kesi nyingine ya uhujumu uchumi Jijini Arusha ya kusafirisha ndege 80 kwenda Jiji la Guangzhou nchini China.
Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 27, Ahmed anatuhumiwa kati ya Januari 1,2005 na Septemba 14,2013 alisafirisha nyara za Serikali kwenda Guangzhou nchini China.
Ilidaiwa na mawakili wa Serikali Elisaria Zakaria na Agustino Kombe katika kipindi hicho, mshitakiwa alisafirisha kwenda China ndege 80 aina ya Pelican wenye thamani ya Dola 4,000 za Marekani.
Fedha hizo ni sawa Sh6.4 milioni za Tanzania na kwamba kosa hilo ni kinyume cha kifungu namba 84(1) cha sheria namba 5 ya uhifadhi wa Wanyamapori ya mwaka 2009.
Pia ilidaiwa kuwa katika kipindi hicho hicho katika mikoa ya Dar Es salaam na Arusha, mshitakiwa aliwinda na kuua aina saba ya Wanyama wenye thamani ya dola 28,520 za Marekani.
Wanyama hao na thamani yake kwenye mabano ni Tembo (Dola 15,000), Chui (Dola 3,500), Duma (Dola 4,900),Nyati (Dola1,900), Pofu (Dola 1,700), Pundamilia (Dola 1,200) na Swala (Dola 320).
Mwisho

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .