ZANZIBAR: KUELEKEA UCHAGUZI WA JUMAPILI, WANAHABARI WATIWA KASHIKASHI

No comments
Saturday, March 19, 2016 By danielmjema.blogspot.com

HALI ya kisiasa visiwani Zanzibar imezidi kuwa tete baada ya vyama viwili vyenye wanachama na wafuasi wengi kutangaza kutovumiliana. Vyama hivyo, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF) kwa nyakati tofauti wiki hii vimetangaza kujibu mapigo katika matukio ya aina yoyote yenye mwelekeo wa kusababisha vurugu dhidi ya wanachama au wafuasi wao ambayo yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa marudio.

Kwa mujibu wa Taarifa iliyochapishwa leo na Gazeti la MTANZANIA, sambamba na hali tete kati ya vyama hivyo, vyombo vya ulinzi na usalama visiwani Zanzibar jana vilimkamata mpiga picha wa Gazeti hili, Silivan Kiwale, wakati akitekeleza majukumu yake ya kikazi na kumwamuru kufuta picha zote alizokuwa amepiga katika eneo la bandari ya Zanzibar.

Kiwale alitiwa nguvuni wakati akipiga picha katika eneo la bandari ya Zanzibar na kuamuriwa na wana usalama hao kufuta picha zote alizokuwa amepiga katika eneo hilo kisha akapewa tahadhari ya kuwa makini na nyendo zake wakati wote atakaokuwa visiwani humo.

Baada ya kufuta picha hizo na kuachiwa, Kiwale alijikuta akikamatwa kwa mara ya pili wakati akifuatilia kitambulisho maalumu cha kazi kinachotolewa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ambapo baada ya kuhojiwa aliachiwa.

Katika tukio jingine mwandishi wa habari wa Shirika la Utangazaji la Ujerumani na Mwakilishi wa Gazeti la Mwananchi visiwani Zanzibar, Salma Said, jana alikamatwa na maofisa usalama akiwa katika uwanja wa ndege wa Zanzibar.

Salma alikamatwa saa 08:05 mchana  muda mfupi kabla ya kuanza safari ya kuelekea Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu. Akizungumzia tukio hilo, mume wa mwandishi huyo aliyejitambulisha kwa jina la Ali, alisema wakati ndege ndogo aliyokuwa akitarajiwa kusafiri nayo Salma aina ya Auric ikijiandaa kuruka, abiria walitangaziwa kwamba ndege hiyo itasubiri kwa muda kabla ya maofisa usalama kuingia na kumkamata.

“Ndege imecheleweshwa karibu nusu saa, abiria wakaelezwa ndege inasubiri kwanza na ndipo walipokuja polisi na kumchukua,” alisema Ali.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis, alipoulizwa kuhusu kukamatwa kwa mwandishi huyo alisema hana taarifa hizo. Salma amekamatwa ikiwa ni siku chache tu baada ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, Salum Msangi, kutoa kauli kwamba polisi ina orodha ya watu 31 wakiwamo waandishi wa habari ambao itawaita kwa kuwahoji kuhusiana na matukio mbalimbali yanayoendelea visiwani Zanzibar yakiwamo ya ulipuaji wa mabomu katika sehemu mbalimbali za Unguja na Pemba.

Tayari polisi wamekwishawahoji Mkuu wa Mikakati wa CUF, Eddy Riyami na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho kwa upande wa Zanzibar, Nassor Mazrui, huku wakiendelea kumshikilia Kaimu Mkurugenzi wa Habari, Mawasiliano ya Umma wa CUF, Hamad Masoud.

TAMKO LA UMOJA WA KLABU ZA WAANDISHI WA HABARI TANZANIA JUU YA KUTEKWA KWA MWANDISHI WA HABARI WA SAUTI YA UJERUMANI ( DW ) SALMA SAID.

Salma Said mwandishi wa DW Zanzibar ametoweka baada ya kutekwa na watu ambao hawajafahamika jijini Dar es salaam, hali ambayo imeleta fadhaa na mshtuko kwa waandishi, jamii na familia yake  hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa marejeo Zanzibar.

Ifahamike kuwa Kazi  ya mwandishi wa habari ni kutoa habari juu ya kila kinachoendelea katika jamii , hivyo kama kuna dosari , dosari hiyo ni ya jamii na sio ya anayeieleza dosari .

UTPC inalaani na kupinga utekaji uliofanywa ambao sababu zake bado hazijulikani, hivyo tunaitaka serikali kuhakikisha Salma Said anatafutwa, kupatikana  na anaachiwa huru mara moja kwa kuwa Serikali ndio yenye jukumu la kulinda raia wake.

Kama utekwaji wa Salma umefanywa kutokana na kazi yake ya uandishi habari tunalaani vikali hatua hiyo, vitendo hivi havipaswi kuendelea katika  nchi inayoheshimu misingi haki na Demokrasia, Vitendo vya namna hii vinadumaza na kufifisha  uhuru wa habari .

Tunapinga kwa nguvu zetu zote  waandishi wa habari kukamatwa na vyombo vya dola au makundi ya kihalifu kwa visingizio ama vya uchochezi au maslahi ya taifa. Waandishi tutaendelea kufanya kazi zetu bila kujali vitisho vya aina yoyote ile kutoka kwa mtu yoyote au Serikali.
 
Imetolewa na
DEOGRATIUS NSOKOLO
RAIS WA KLABU ZA WAANDISHI WA HABARI TANZANIA -UTPC.
March 19, 2016.
 

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .