GAMA AWAONDOA HOFU WANANCHI KUHUSU USALAMA WA SIRI ZAO KATIKA SENSA

Posted in
No comments
Sunday, July 29, 2012 By danielmjema.blogspot.com

Leonidas Gama-mkuu wa mkoa wa kilimanjaro
 MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama amevitaka vyombo vya Dola kuhakikisha vinaongeza usalama katika kipindi hiki cha sensa kama njia ya kuondoa wasiwasi uliotanda miongoni mwa wananchi kuhusu usalama wa zoezi hilo.
Gama Alitoa kauli hiyo katika kikao cha dharura na Waandishi wa Habari kilichofanyika Ofisini mwake jana kwa lengo la kujadili na kuangazia mambo mbalimbali ikiwemo zoezi la kuhesabu watu na makazi ambayo imepangwa kufanyika usiku wa kuamkia Agosti 26.

Alisema ipo haja ya Kamati ya Ulinzi na Usalama katika kila Wilaya ikishirikiana na Jeshi la Polisi kuhakikisha swala la Ulinzi na Usalama wa Raia unapewa kipao mbele, hasa katika kipindi hiki cha Sensa, kutokana na kuwepo kwa hofu ya shughuli hiyo kutoa Mwanya kwa wahalifu kuhatarisha usalama wa Raia.

“Natoa agizo kwa kamati ya Ulinzi na Usalama katika kila Wilaya kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kuhakikisha kwamba Usalama wa Raia katika kipindi hiki cha Sensa kinapewa kipaumbele na umuhimu mkubwa kuliko vipindi vingine vyote,kuna watu wanataka kutumia zoezi hili kutekeleza uhalifu wao,hilo hatutaliruhusu hata kidogo ” alisema Gama.

Aidha Gama aliwataka wakuu wote wa kila kaya kutunza kumbukumbu muhimu kama vile Umri, Jina, Jinsia, Kiwango cha Elimu, Uraia, Shughuli za kiuchumi, mahali anapoishi na kushinda, kama ameolewa au ameowa na watoto, za watu walioamkia katika kaya yake kutokana na vitu hivyo kuwa mahitaji muhimu katika kutathmini Maendeleo ya sehemu husika.

Alisema kuwa taarifa zitakazokusanywa kutoka kwa Wananchi zitatunzwa kwa matumizi yakitakwimu tu kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu Namba 1 ya mwaka 2002, hazitatolewa kwa Mtu yeyote Yule na kusisitiza kwamba , Usiri wa Taarifa hizo utazingatiwa na hivyo kuwaondoa hofu wananchi kuhusu uwezekano wa siri zao muhimu kuvujishwa kwa matumizi yasiokusudiwa.

“Nawakikishia Wananchi kuwa, Taarifa watakazo toa zitatunzwa  kwa siri na zitatumika kwa Shughuli za kitakwimu tu, hii ni kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu, namba 1 ya mwaka 2002,”alisema Gama.

Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, aliwataka Wananchi kuendelea na Shughuli zao za Kiuchumi kama kawaida wakati wote wa zoezi la kuhesabu Watu na Makazi kutokana na zoezi hilo kutoathiri shughuli za kiuchumi za Mkoa huku akikemea vikali Tabia ya Watu kubweteka kwani ili Juhudi za kunyanyua uchumi wa Nchi zifanikiwe, inabidi watu kujituma kwa Nguvu zote na kwa nyakati zote.

Kwa upande wake, Mratibu wa Sensa Mkoa wa Kilimanjaro, Alex Luwavi, alibainisha kwamba swala la Usalama wa Wananchi umezingatiwa kwa kuhakikisha kwamba Makarani wote watapewa Vitambulisho na Sare maalumu zitakazo watambulisha kama njia ya kuziba mianya inayoweza kutumiwa na Watu wasio waaminifu na kusabibabisha madhara kwa Jamii.

Pia aliwataka Wawezeshaji wapatao 186, waliomaliza mafunzo yaliochukua takribani wiki mbili na kufungwa  mwishoni mwa wiki hii, kutoa mafunzo kwa Makarani wote watakaochaguliwa na kuwasisitiza, kufanya kazi kwa uadilifu na kwa Bidii kutokana na umuhimu na ugumu wa kazi hiyo ili kuwezesha zoezi hili kufanikiwa kwa asilimia kubwa.

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .