MAMA ALIYEJIFUNGUA "MAPACHA WANNE" KCMC AOMBA MSAADA

Posted in
No comments
Monday, September 23, 2013 By danielmjema.blogspot.com


Mkuu wa wilaya ya Same, Herman Kapufi akimjulia hali mama, Nipa Mrutu  (36), aliyejifungua watoto wanne, alipomtembelea juzi katika Hospitali  ya rufaa ya KCMC, iliyoko mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.Mama huyo  alijifungua watoto hao Septemba 10 mwaka huu.

Mkuu wa wilaya ya Same, Herman Kapufi (aliyevaa suti nyuesi),  akimjulia hali mama, Nipa Mrutu (36), aliyejifungua watoto wanne,  alipomtembelea juzi katika Hospitali ya rufaa ya KCMC, wa pili ni  Mkurugenzi wa Huduma za Afya wa KCMC, Prof. Moshi Ntabaye pamoja na  baadhi ya wauguzi wanaomuhudumia Mama huyo.Mama huyo alijifungua  watoto hao kwa njia ya Upasuaji Septemba 10 mwaka huu.



Na Mwandishi Wetu, Kilimanjaro


MWANAMKE aliyejifungua mapacha wanne katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC  ameiomba Jamii ya Watanzania kumsaidia fedha za kugharamia malezi ya  watoto hao kutokana na hali yake kiuchumi kumuwia vigumu kuwapa watoto  hao malezi stahili.
Mwanamke huyo aliyefahamika kwa jina la Nipa Mrutu (36), mkazi wa  kijiji cha Kavambugu, Kata ya Same mjini, wilaya ya Same, mkoani  Kilimanjaro, alilazwa katika hospitali hiyo, Agosti 3 na kujifungua  watoto wanne kwa njia ya Upasuaji Septemba 10 mwaka huu.

Akizungumza na Waandishi wa Habari katika wodi ya kina Mama hospitalini  hapo, Mrutu ambaye ni Mkulima na mama wa Watoto saba pamoja na uzao  huo, alisema kuwa kutokana na hali yake kiuchumi kuwa duni hatoweza  kugharamia mahitaji ya malezi ya wanae.

Alisema kwa hivi sasa, ukiacha gharama za kuwalea watoto hao pia  anadaiwa Hospitalini hapo fedha ambazo ni nyingi sana na hivyo anatoa  wito kwa yeyote yule atakayeguswa na hali yake kumsaidia chochote  kitakacho mwezesha kukidhi mahitaji ya watoto hao.

“Namshukuru Mungu nimejifungua salama, lakini kwa kweli sijui hawa  wanangu nitawaleaje, mimi ni mkulima, kipato changu pamoja na mume  wangu hakituwezeshi kuwalea watoto wetu, tangu Tarehe 3 mwezi wa nane  niko hapa, bili ni kubwa mno,” alisema Mrutu.

Kwa upande wake Mkuu wa idara ya akina Mama katika Hospitali ya KCMC,  Dkt. Gileard Masenga alisema kuwa baada ya kumfanyia mwanamke huyo  uchunguzi wa Kitabibu, walilazimika kumzalisha Septemba 10 ikiwa ni  wiki 34 tu za ujauzito wake.

Dkt. Masenga alisema kitaalam, inatakiwa  mwanamke abebe mimba kwa muda wa wiki 40 lakini kutokana na Mgonjwa  wao kuonekana kuwa na shinikizo la Damu Uongozi wa Hospitali iliamua
afanyiwe upasuaji kuokoa maisha ya viumbe vilivyoko tumboni.

Alisema katika taarifa za madaktari, afya ya mwanamke huyo ilionekana  kuzorota kutokana na shinikizo la damu lililokuwa likimsumbua  kuongezeka mara kwa mara hali ambayo iliwalazimu kumpa dawa maalum kwa  ajili ya kuboresha afya ya Mama na watoto.

“Kitaalam inatakiwa Mama mjamzito ajifungue baada ya wiki 37 kwani  hapo mapafu ya mtoto yanakuwa yamekomaa, hali ilikuwa tofauti kwa  mgonjwa wetu, Presha yake ilikuwa inapanda kila kukicha hivyo tukaamua  kumpa dawa maalum ambayo itasaidia kukomaza mapafu ya watoto”, alisema  Dkt. Masenga.

Kuhusu hali ya Watoto hao kiafya Dkt. Masenga alisema watoto hao ambao  watatu ni wa kiume na mmoja ni wa kike, walizaliwa na uzito wa  kilogramu 1.5, wa pili 1.6 watatu ambaye ni wa kike ana 1.8 huku wanne  akiwa na uzito wa kilogramu 1.6 wana afya nzuri japo kwa sasa wako
katika uangalizi wa madaktari.

Alisema kutokana na uzito wao kutofikia uzito unaotakiwa wa kilogramu  angalau 2.5 au zaidi, wameamua kuwaweka katika wodi maalum na  kuwatenga na Mama yao hadi hapo uzito wao utakapoimarika huku  akibainisha kuwa hiyo ni salama kwao kutokana na magonjwa ya
maambukizi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Same, Herman Kapufi, aliyefika Hopitalini hapo  Juzi kumjulia hali Mama huyo na wanaye wanne, alisema tayari serikali  ya Wilaya ya Same imeshaanza kufanya utaratibu wa kuhakikisha Mama  huyo anapata msaada.

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .