TANZANIA: WIZI MKUBWA BODI YA MIKOPO-HELSB

Posted in
No comments
Wednesday, February 17, 2016 By danielmjema.blogspot.com

WAZIRI WA ELIMU, dKT. JOYCE NDALICHAKO

Wakati migomo ya wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu mbalimbali nchini ikiendelea ulitikisa Taifa, uongozi wa Bodi ya Mikopo nchini (HESLB), umefuja Sh. bilioni 3.23 za mikopo ya wanafunzi kwa kutoa mikopo hewa, kulipa waliomaliza vyuo, ambao hawajaomba mikopo huku wengine wakilipwa mara mbili mbili.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, alisema ubadhirifu wa fedha hizo ulibainishwa na Mkaguzi wa Ndani alipokagua hesabu za bodi hiyo mwaka 2013, lakini mpaka sasa ripoti hiyo ilikuwa imefungiwa kabatini bila kufanyiwa kazi.

Alisema baada ya kuingia ofisini, bodi hiyo waliandikiwa barua ili kujibu hoja zilizobainishwa na mkaguzi huyo, badala ya kujibu hoja walijikita kulalamika kuwa Mkaguzi wa Ndani aliingia kazi ambayo ingetakiwa kufanywa na Mkaguzi wa Bodi.

Kufuatia kutoridhishwa na majibu hayo, alisema ofisi yake imeamua kumfuta kazi Mkurugenzi Mtendaji wa bodi hiyo, George Nyatenga.

Mbali na Mkurugenzi huyo, Profesa Ndalichako alisema ofisi yake imewasimamisha kazi Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Yusuf Kisare, Mkurugenzi wa Urejeshaji Mikopo, Juma Chagonja na Mkurugenzi wa Upangaji na Utoaji Mikopo, Onesmo Laizer.

Alisema kwa kuwa Nyatenga alishastaafu na alikuwa akifanya kazi kwa mkataba ambao ungeisha Agosti, mwaka huu, baada ya kuuvunja kwa notisi ya siku moja, Mkurugenzi huyo atalipwa mshahara wa mwezi mmoja kwa mujibu wa sheria ya utumishi wa umma.

Kwa Wakurugenzi wengine watatu waliosimamishwa, Profesa Ndalichako alisema watakaa nje ya ofisi na wizara yake itateua maofisa wa kwenda kushika nyadhifa zao kwa muda ambao Mkaguzi wa Ndani atarudi tena kukagua hesabu za tangu mwaka 2013 mpaka sasa.

FEDHA ZILIVYOTAFUNWA
Profesa Ndalichako alisema katika ukaguzi huo, ilibainika kuwa wanafunzi 23 walilipwa mikopo kupitia vyuo viwili tofauti kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo.

Alisema katika chuo cha kwanza, wanafunzi hao walilipwa Sh. milioni 153.9 na kwenye chuo cha pili Sh. milioni 147.54.
Katika eneo lingine, alisema wanafunzi 169 walipata mikopo kupitia vyuo viwili tofauti kwa miaka miwili mfululizo ambapo kwenye chuo cha kwanza Sh. milioni 658.04 zilitolewa huku kwenye chuo cha pili zikitolewa Sh. milioni 665.13.

Profesa Ndalichako alisema bodi hiyo pia ilitoa Sh. milioni 342.46 kwa wanafunzi 343 ambao usaili wao haupo kwenye vyuo ambavyo fedha hizo zimepelekwa.

Profesa Ndalichako alisema bodi hiyo pia ililipa Sh. milioni 136.23 kwa wanafunzi 55 ambao wameacha masomo.

“Sh. milioni 159.66 zililipwa kwa wanafunzi 306 zaidi ya kiwango kinachokubalika kisheria,” aliongeza Profesa Ndalichako.

Alitaja kundi lingine kuwa ni lile la wanafunzi ambao walilipwa fedha kwenye vyuo vya ndani na nje ya nchi kwa wakati mmoja.

Katika kundi hilo, alisema wanafunzi 77 wawalilipwa Sh. 467.62 kwenye vyuo vya nje ya nchi na wakati huo huo wakilipwa Sh. milioni 123.04 kwenye vyuo vya ndani ambavyo walikuwa hawasomi.

Alisema pia kuwa Sh. milioni 207.05 zilipelelekwa kwenye vyuo sita na hazikuchukuliwa na wanafunzi na kiutaratibu zingepaswa kurudishwa Bodi, lakini ziliyeyuka.

Alisema pia kwamba, wanafunzi 143 walilipwa Sh. milioni 173.64 katika muda ambao walikuwa hawajasajiliwa kwenye vyuo husika. 

Bila kutaja kiasi cha fedha kilicholipwa, alisema ripoti hiyo ya Mkaguzi wa Ndani iliainisha kuwa wanafunzi 19,348 walipewa mikopo ambayo haijapitishwa na Bodi ya Kamati ya Mikopo, jambo ambalo ni kinyume cha taratibu.

Pia alisema wanafunzi 54,299 walipangiwa mikopo wakati walikuwa hawajaomba.

“Wakati kukiwa na watoto wa maskini wanaomba mikopo na hawapewi, wengine bila hata kuomba wanapewa, hili halikubaliki,” alisisitiza Profesa Ndalichako.

Kutokana na hali hiyo, Profesa Ndalichako alisema utendaji mbovu na ubadhirifu umesababisha kuwe na malalamiko kutoka kwa wanafunzi kila wakati.

Alisema wakati mwingine, wanafunzi wanavyolalamika na wizara kuingilia kati, hulipwa fedha zao ndani ya siku moja ama mbili, jambo linaloonyesha kuwa siyo kweli kwamba kuna tatizo la fedha.

Alisema kutokana na usumbufu huo usio wa lazima, wanafunzi wa Vyuo Vikuu vya St. Joseph Songea, St. Joseph Arusha, Chuo Kukuu cha Dodoma (Udom) na wanafunzi wengine mmoja mmoja kutoka kwenye vyuo vingine, waliwasili vyuoni mwao Novemba, 2015, lakini walipewa mikopo Januari, mwaka huu.

“Wanafunzi wanaosoma nje ya nchi kama Ujerumani na  Algeria, wamekuwa wakiendelea kulipwa fedha wakati muda wa mkataba wao wa mikopo umeisha,” alifafanua.

Alisema baadhi yao wameendelea kulipwa huku wakiwa wamemaliza masomo na kuendelea na kazi kwenye nchi walizokuwa wakisoma na wengine wakiendelea na masomo ya juu tofauti na mikataba yao ya awali ilivyokuwa inataka.

“Licha ya udhaifu uliobainishwa na Bodi kutakiwa kujibu hoja hizo, haikutoa majibu kwa Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali hadi Januari, 2016 ilipoagizwa na Wizara kufanya hivyo.

Majibu yaliyowasilishwa na Bodi Februari mosi, mwaka huu, yanadai Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, hakukidhi viwango na alijikita kwenye mambo ya uendeshaji wakati kazi hiyo hufanywa na Mkaguzi wao wa Ndani,” alisema Profesa Ndalichako. 

ZINGESOMESHA WANAFUNZI 808
Fedha hizo ambazo zimelipwa kinyume cha taratibu, zingesomesha wanafunzi 808 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Wanafunzi hao ni wale ambao wakilipiwa asilimia 100 ya mkopo kwenye ada, fedha za kujikimu, za vifaa vya kujifunzia na zile za mazoezi kwa vitendo na nyingine zote ambazo zingehitajika, kila mmoja angepata Sh. milioni nne na akasoma kwa mwaka mzima bila kudaiwa chochote.

Baadhi ya fani ambazo wastani wa gharama yake unaakisi kiasi hicho cha fedha kwenye Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni pamoja na ile ya Mawasiliano kwa Umma, Uhusiano kwa Umma na Uandishi wa Habari.

Wanafunzi hawa ambao hulipwa Sh. 8,500 kwa siku kwa ajili ya chakula na malazi, kwa muhula hulipwa wastani wa Sh. milioni 1.2 ada ya mwaka Sh. milioni 1.3, huku kiasi kingine kikienda kwenye mafunzo kwa vitendo na mahitaji mengine. 

NA FREDY AZZAH
CHANZO: NIPASHE

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .