THE RISE AND FALL OF ABOUD JUMBE MWENYE (sehemu ya tatu)

No comments
Sunday, April 10, 2016 By danielmjema.blogspot.com

KATIKA sehemu ya pili ya makala haya, tuliona namna Rais wa awamu ya pili wa Zanzibar, Sheikh Aboud Jumbe Mwinyi, alivyoandaa mashtaka dhidi ya Jamhuri ya Muungano, akihoji uhalali wa Muungano kwenye Mahakama Maalum ya Kikatiba. 



Tuliona pia namna hati hiyo ya mashitaka ilivyopotea mezani kwake Ikulu katika mazingira ya kutatanisha, na hatimaye alivyopata kibano cha Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM na kuvuliwa nyadhifa zake zote za uongozi kichama na kiserikali.

Tuliona pia namna ilivyokuwa kazi ngumu kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kuteua mrithi wake muda wake wa kung’atuka ulipowadia, kutokana na kambi mbili zenye nguvu sawa ndani ya Kamati Kuu (CC) na NEC ya CCM kuumana, hata akateuliwa Ali Hassan Mwinyi, kinyume na matarajio ya Mwalimu Nyerere ambaye chaguo lake lilikwa ni Balozi Salim Ahmed Salim. 

Kambi hizo mbili, zote za Kizanzibari, kwa majina zilijulikana kama ‘Kambi ya Wakombozi’ (Liberators) iliyotaka kudumishwa kwa sera na fikra za Mzee Abeid Amani Karume, Rais wa kwanza wa visiwa hivyo, kama njia ya kulinda Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964. 

Kambi hii, ilitaka misingi ya Muungano irejewe upya na kuundwa kwa Shirikisho lenye Serikali tatu; Serikali ya Tanganyika, Zanzibar na Serikali ya Shirikisho. Kambi ya pili ilijiita ‘Wanamstari wa Mbele’ (Frontliners), iliyotaka mabadiliko katika sera na fikra za Mzee Karume visiwani ili kuleta demokrasia na utawala bora.

 Aidha, kambi hii ilitaka kuimarishwa kwa Muungano kwa muundo ulivyo sasa.  Kambi ya ‘Wakombozi,’ kwa kuunganisha nguvu na wajumbe wa CC na NEC wa Bara, wakiongozwa na kuunganishwa na kiongozi wao mkubwa, Mzee Paul Bomani na Mama Getrude Mongella, ilishinda.

Nilikusudia kumaliza makala yangu na sehemu hiyo ya pili, lakini kutokana na maombi na kilio cha wasomaji wangu cha kwamba niendeleze makala haya, nimekubali kufanya hivyo. Sasa tuendelee na sehemu hii ya tatu na ya mwisho.

‘Wakombozi’ wapeta tena uteuzi Rais wa Zanzibar

Uteuzi wa Mwinyi kugombea nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano, uliofanywa na NEC chini ya mfumo wa chama kimoja, ulikuwa tiketi turufu kwa mteule huyo kushika nafasi hiyo. Kwa jinsi hii, nafasi ya Rais wa Zanzibar aliyokuwa ameshikilia ikawa imebaki wazi.

Wakati wa kupendekeza jina ndani ya Kamati Kuu (CC) ulipowadia, ‘Wakombozi’ walikuwa wepesi kupendekeza kwa sauti moja na kwa pamoja. “Abdul Wakil Nombe.” Wakil  alikuwa Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar wakati huo. Nayo kambi ya ‘Wanamstari wa Mbele’ ikapendekeza jina la Seif Sharrif Hamad, ambaye alikuwa Waziri Kiongozi wakati huo.

Majina yaliyopendekezwa na CC kwa nafasi za Rais wa Jamhuri ya Muungano na Rais wa Zanzibar, yaliwasilishwa NEC kwa ajili ya kupigiwa kura kupata wagombea, Agosti 15, 1985. Kwa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano, liliwasilishwa jina la Ali Hassan Mwinyi; na kwa nafasi ya Rais wa Zanzibar, yaliwasilishwa majina ya Abdul Wakil Nombe na Seif Sharrif Hamad.

Nyerere akwaa kisiki tena kuhusu mrithi

Kwa kumtumia Sheikh Thabit Kombo Jecha, aliyekuwa mjumbe wa CC na NEC ya CCM mwenye nguvu ndani ya CCM, Mwalimu alitupa kete yake ya mwisho kuhakikisha kwamba jina la Mwinyi halivuki kihunzi cha NEC, ili jina la Dk Salim Ahmed Salim ambalo halikuwasilishwa na CC ndani ya NEC, liibuke na kupitishwa. Lakini mambo hayakuwa rahisi, na ikiwa kinyume na alivyotarajia.

Kwa kuanza, Sheikh Thabit Kombo alionyesha wasi wasi wake na kwa Chama, kama Rais Mwinyi wa Zanzibar, ambaye alionyesha mafanikio makubwa kiutawala Visiwani kiuchumi na kisiasa na kwa kuleta utulivu katika kipindi kifupi cha miezi kumi na minane tu ya utawala wake, hivi kwamba kuondoka kwake kungeirudisha Zanzibar kwenye enzi mbovu za awamu mbili zilizotangulia, yaani awamu ya Abeid Karume na awamu ya Jumbe.

Sheikh Kombo alizomewa na kauli yake ikazamishwa na kelele za wajumbe wa NEC kutoka Bara wakimkatalia.  Ni Khatib Hassan pekee wa kambi ya ‘Wanamstari wa Mbele,’ aliyekuwa jasiri vya kutosha kumuunga mkono Kombo. Majadiliano makali yakafuata lakini bila suluhu.
Mwalimu Nyerere akaahirisha kikao, kisha akawaita pembeni kwa siri, Mzee Mwinyi, Mzee Kawawa na Sheikh Kombo na maswahiba wake wachache. 

Sheikh Kombo, baada ya kikao hicho cha siri, kwa mshangao wa wengi, alikuwa amegeuka tayari kumuunga mkono Mzee Mwinyi kwa nafasi ya Rais wa Jamhuri; na kwa mara ya kwanza, akamuunga mkono Wakil kwa urais wa Zanzibar. Kura za ‘Ndiyo’ au ‘Hapana’ zikapigwa kwa mgombea pekee wa urais wa Jamhuri ya Muungano, Ali Hassan Mwinyi.

Kati ya kura 1,732 zilizopigwa, ni kura 14 tu ndizo zilizomkataa Mwinyi. Ikafuata zamu ya Wakili na Hamad. Katika vuta nikuvute hiyo, Wakil akaambulia ushindi mdogo wa kura 85 dhidi ya kura 78 za Hamad. Ushindi wa nafasi zote mbili hizo, kwa kiasi kikubwa uliwapagawisha ‘Wanamapinduzi’ na kuwahuzunisha ‘Wanamstari wa Mbele,’ huku wakiulizana bila kupata jibu, kama kweli Mwalimu alikuwa upande wao tangu mwanzo.
 
Sheikh Hassan Nassoro Moyo na marafiki zake, walisherehekea ushindi huo wazi wazi, huku Getrude Mongella akisikika akijigamba kuwa ni wao (yeye na wenzake) waliompendekeza Mwinyi na Wakil kwenye CC na kuokoa jahazi. Wapinzani wa Dk Salim Ahmed Salim kutoka Tanzania Bara, walifarijika na kupumua kuona Mwinyi ameteuliwa kugombea urais, kwa kuwa walimwona anaingilika kwa urahisi kuliko Dk Salim mwenye kujiamini na makini katika kusimamia mambo na kwa maamuzi.

Hata hivyo, taarifa za kiinteligensia zilionyesha kwamba Wakil asingeweza kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura katika uchaguzi mkuu kwa jinsi ambavyo hakukubalika visiwani, ikilinganishwa na Hamad, kama angeteuliwa.  Na kama ingetokea Wakil kutoshinda, chama kingelazimika kuteua mgombea mwingine, na pengine Seif Sharrif Hamad huyo huyo.

Ili kuokoa jahazi, Mwalimu na Mwinyi walimwita Hamad pembeni karibu mara tatu kumwomba ampigie kampeni Wakil, na hasa kisiwani Pemba. Kwa upande wake, Hamad alipoitwa na kina Mwinyi akahoji akisema:  “Iweje niombwe kufanya hivyo wakati baadhi ya wajumbe wa NEC wanapita mitaani wakijiita ‘Washindi’ na mimi ‘Mchakazwa,’ na kwamba eti wamemweka Wakil kupindua Serikali ya awamu ya tatu (ya Mwinyi) visiwani; na zaidi eti kwamba Wakil ataitawala Zanzibar vyema kwa staili ya ASP?”

Malalamiko ya Hamad yalimwingia Mwalimu Nyerere, kisha akamwita Dk Salmin Amour na kumwambia:  “Ninazo taarifa zote, kwamba wewe unajiandaa kwa kujidanganya kuchukua nafasi ya Waziri Kiongozi; unajitangaza eti wewe ni Mkombozi. Umemkomboa nani kama si kuwagawa Wazanzibari?”

Sheikh Natepe, bila kujali msimamo wa Mwalimu dhidi ya Dk Salmin, aliingilia kati kwa kupinga yaliyokuwa yakitokea visiwani. Kwa sauti ya ukali alisema: “Siwezi kufanya kazi na mwanachama yeyote wa zamani wa Chama cha Zanzibar Nationalist Party (ZNP), Zanzibar and Pemba People’s Party (ZPPP) au Umma Party na ndugu zao. Watu hawa kamwe hawawezi kuchukua nafasi za madaraka nikiwa bado hai katika nchi hii kwa sababu (hao) ni maadui wa watu wa Zanzibar wanaotaka kulipiza kisasi kwa ASP.”

Mwalimu Nyerere alijitahidi kumnyamazisha Sheikh Natepe kwa maneno makali: “Najua, wewe ni kiongozi wa njama hizi, unalo kundi; najua.” Dk Salim Ahmed Salim, ambaye muda wote huo alikuwa kimya akisikiliza, alisimama na kuelezea masikitiko yake juu ya msimamo wa Sheikh Natepe, akaelezea nyadhifa nyingi alizoshika katika kuitumikia Zanzibar na Jamhuri ya Muungano, na utii wake wa miaka 21 kwa Mwalimu, Chama na Serikali.

Alisema Dk Salim: “Muda wote nimekuwa rafiki kwa kila mtu na sijamdharau mtu yeyote. Kwa hiyo, nashangaa kujiona nakuwa shabaha ya mchezo huu mchafu wa kisiasa na uvumi wa kuchafuliana hadhi. Kama huu ndio mwenendo katika uongozi wa Chama (CCM), basi niko tayari kuachia ngazi zote ndani ya Chama na Serikali, na sitagombea ubunge.”

Mwalimu Nyerere akasituka. Ni Mwinyi aliyeokoa jahazi Dk Salim asiachie ngazi, kwa kuishambulia kambi ya Sheikh Natepe kwa kuhubiri na kutenda ubaguzi wa rangi. Na wakati wa kuhitimisha kikao hicho kifupi, Mwalimu Nyerere alibadili makasia akisema: “Nataka muelewe kwamba nawaelewa vyema vijana hawa (Wanamstari wa Mbele). Ni vijana wakweli na si wasaliti, wala si wahaini. Sitavumilia kusikia wakiitwa au kutendewa kama maadui.”

Kwa karipio hilo la Mwalimu Nyerere, kambi ya Sheikh Natepe ikanywea na mmoja wao, Ali Mzee, akaomba radhi. Kwa hiyo, ikaazimiwa kwamba Mwalimu, Mwinyi, Kawawa, Dk Salim na Hamad, waanzishe kampeni kumsaidia Wakil ashinde. Akiwa Wete (Pemba), Mwinyi alinukuliwa akiwaponda ‘Wakombozi’ akisema: “Hawa wajinga wanaojiita Wakombozi, wanaotaka kuirejesha Zanzibar na Wazanzibari kwenye maovu ya utawala wa enzi za Sheikh Karume; wakataeni, msiwasikilize!”

Katika uchaguzi huo, licha ya kampeni kubwa, Wakil aliweza kupata asilimia 58.6 tu ya kura zilizopigwa. Mkasa ukawapata pia wagombea wengi wa Baraza la Wawakilishi waliojipambanua na kambi ya ‘Wakombozi’ kwa kushindwa vibaya katika uchaguzi huo.
Lakini kwa yote hayo, ‘Wakombozi’ ndio waliokuwa washindi kwa kufanikiwa kuweka madarakani marais wa sehemu zote mbili za Muungano.

Mpambano wa kambi hizi mbili, ulibadilika pale baadhi ya ‘Wanamstari wa Mbele’ wakiwano Sheikh Sepetu, Ali Ameir Mohamed na Adam Mwakanjuki, walipojiengua na kujiunga na kambi ya ‘Wakombozi’ na hivyo kudhoofisha kabisa kambi ya ‘Wanamstari wa Mbele.’
Kwa kutumia mwanya huo, Wakil alivunja Baraza la Mawaziri na kuteua Makatibu Wakuu kuongoza Serikali.

Na alipoteua Baraza la Mawaziri jipya, Hamad na ‘Wanamstari wa Mbele’ wenzake hawakuwamo. Mwaka mmoja baadaye, Mkutano Mkuu wa CCM uliofanyika Kizota, Dodoma, uliwafukuza na kuwavua uanachama, Shaaban Mloo, Ali Haji Pandu, Khatib Hassan, Soud Yusuf Mgeni, Hamad Rashid na wengineo.

Kwa kufanya hivyo, CCM kilidhani kilikuwa kinatua mzigo wa ‘wakorofi’ hao wachache, lakini badala yake waliungana na kujipanga upya na kuanzisha upinzani imara wa kisiasa nje ya Chama na Serikali na kuitikisa CCM na Serikali yake. Kwa sababu hiyo, Hamad na wenzake hao walikamatwa na kutiwa kizuizini, na baadaye kushtakiwa kwa kutaka kupindua ‘dola’ ya Zanzibar.

Na kufuatia kushinda kesi hiyo, Hamad na wenzake walianzisha kikundi cha chini kwa chini cha mapambano ya kisiasa kilichofahamika kwa jina la Kamati ya Mwelekeo wa Vyama Huru (Kamahuru), kama msingi tangulizi wa kuzaliwa kwa Chama cha Wananchi (CUF). 

Kufikia hapo, ni dhahiri kwamba mtizamo wa wana-CCM Zanzibar, ni ndoto ile ile ya ‘Wakombozi’ ya kutaka kutawala kwa staili ya ASP ya enzi za Mzee Karume, wakati mtazamo wa CUF ni kuona sera za ASP na Karume zinatoweka ili kupata Zanzibar mpya. 

Je; Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK), ina ubavu wa kuzivunja na kuzizika fikra za kambi hizi mbili kinzani na kufikisha tamati historia ya mifarakano ya kisiasa Zanzibar?

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .