POLISI YAMSHIKILIA ALIYEMUUA HAWARA KIKATILI KILIMANJARO

No comments
Monday, February 10, 2014 By danielmjema.blogspot.com


Mwandishi wetu, Moshi

Polisi mkoani Kilimanjaro inamshikilia mfanyabiashara mmoja wa mjini Moshi baada kumuua kikatili mpenzi wa nje (hawara) kwa Rato baada ya mwanamke huyo kukataa kumpa penzi.

 Mwanamke huyo alikataa kumpa penzi hawara yake huyo ambaye ni mume wa mtu, akitaka ampe kwanza Sh10,000 kwani katika muda wa miaka miwili ya mahusiano yao hakuwahi kumpa kitu.

Kamanda wa Polisi mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz jana alithibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa ambaye baada ya kumuua mpenzi wake, Sekunda Mushi(42), alitupa maiti yake kwenye shimo la taka.

Mtuhumiwa huyo ni baba mwenye familia ya watoto wawili na ana mke wake wa ndoa na wanaishi eneo la Kiborlon mjini Moshi na alikuwa na uhusiano wa siri wa kimapenzi na marehemu.

Tukio hilo ambalo limekuwa gumzo katika mitaa mbalimbali ya mji wa Moshi, lilitokea wiki iliyopita usiku wa manane katika eneo la Kosata katika kijiji cha Longuo A nje kidogo ya mji wa Moshi.

“Huyo mtuhumiwa alimchukua mpenzi wake (marehemu) wakaingia chumbani lakini wakahitilafiana … marehemu alikuwa anataka apewe pesa lakini mwanamme akawa hataki”alisema Kamanda Boaz.

Habari zaidi zimedokeza marehemu alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mtuhumiwa kwa takribani miaka miwili mfululizo na katika kipindi chote, alikuwa hajawahi kumpa pesa yoyote mpenzi wake huyo.

“Siku hiyo usiku walipoingia chumbani mwanamke akamwambia kwa miaka yote hujawahi kunipa hata shilingi moja leo sikupi penzi mpaka unipe Sh10,000”alidokeza polisi mmoja wa upelelezi.

Mara zote wakifanya mapenzi ndani ya chumba cha mfanyakazi wa Grosari yake iliyopo Longuo A, mfanyakazi huyo alikuwa akilala kitanda kimoja na wapenzi hao wawili akishuhudia mapenzi yao.

Akimkariri mfanyakazi Polisi huyo, alidai kitendo cha kupewa sharti hilo la kutoa Sh10,000 angalau kwa siku hiyo ndani ya miaka miwili ya mahusiano yao kilionekana kumuudhi mtuhumiwa.

“Yule jamaa akaanza kumpiga kipigo cha nguvu na kama haitoshi akachukua Rato yenye meno matatu na kumpiga nayo kichwani ikaangia na kutokea mdomoni kwa chini”alidokeza polisi huyo.

Inadaiwa kuwa, mtuhumiwa alimgeuza mwanamke huyo na kuendelea kumpiga na rato mgongoni mithili ya mtu anayelima shamba na kisha kumburuza na kumtupa kwenye shimo la taka.

“Wakati yote hayo yakiendelea Yule mfanyakazi wake alikuwa akishuhudia na alipomtupa kwenye shimo la takataka akamtisha mfanyakazi wake kuwa kama atamweleza mtu naye angemuua”alisema.

Kwa mujibu wa Polisi huyo, baadae mtuhumiwa alimwamuru mfanyakazi wake huyo kwenda kuificha Rato iliyotumika katika mauaji hayo juu ya dari ya chumba hicho ili kuficha uhalifu wake huo.

Baadae mtuhumiwa aliondoka kwenda kijijini kwao huko Marangu Moshi Vijijini hadi alipokamatwa na wananchi na alipoulizwa kuhusu mauaji hayo alikana na ndipo akapelekwa kituo kikuu cha Polisi.

Afisa mtendaji wa kijiji cha Longuo A, Marcel Benard Mushi, alisema waligundua kuwapo kwa mwanamke katika shimo la taka saa 11:00 alfajiri na wakati huo bado alikuwa yupo hai.

“Tulimkuta katika hali mbaya alikuwa na majeraha ambayo kwa kweli huwezi kuamini yametokana na mwanadamu na aliomba maji ya kunywa lakini kabla hatujampatia akakata roho”alisema Mushi.

Kaka wa marehemu, Goodluck Mushi alisema dada yao alikuwa ameondoka nyumbani kwa siku mbili mfululizo na walikuwa wakimtafuta hadi walipopewa taarifa saa 3:00 asubuhi kuwa ameuawa.

Ndugu huyo anasema wanavyofahamu wao, siku alipouawa ndio ilikuwa mara ya kwanza kwenda kwenye Grosari inayomilikiwa na marehemu na ndio siku ambayo walianza uhusiano na mtuhumiwa.

Mazishi ya mwanamke huyo yalifanyika juzi Jumapili baada ya mwili wake kufanyiwa uchunguzi na madaktari wa hospitali ya rufaa ya KCMC ili kubaini nini hasa chanzo cha kifo chake.

Mwisho

Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .