WATU WATATU WAKAMATWA TUHUMA ZA KUSAFIRISHA WATOTO 10 MKOANI KILIMANJARO

Posted in
No comments
Wednesday, June 6, 2012 By danielmjema.blogspot.com



JESHI la polisi Mkoani Kilimanjaro linawashikilia watu watatu (3), kwa tuhuma za kusafirisha na kuwatumikisha watoto wenye umri chini ya miaka 15, kwa ajili ya kulima na kupalilia matuta ya vitunguu wilayani Same, Mkoani Kilimanjaro.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa kwa vyombo vya habari, kamanda wa polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz, alisema jeshi hilo lilipata taarifa kutoka kwa raia mwema, kwamba kuna watoto 10 waliochini ya miaka 15 wamehifadhiwa katika nyumba ya kulala wageni ya Madevoshini, zilizoko DSm street, Manispaa ya Moshi, Mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya kusafirishwa kwenda wilayani Same eneo la Marwa kwa ajili ya kutumikishwa kwenye mashamba ya vitunguu.

Boaz alisema kwamba baada ya kupokea taarifa hizo hatua za haraka zilichukuliwa kufuatilia taarifa hizo na kukuta watoto 10 (majina yamehifadhiwa) na baada ya uchunguzi iligundulika kwamba watoto hao walichukuliwa kutoka kijiji cha Longoi Nguzo Nne, Kikavu chini, Wilaya ya Hai, mkoani Kilimanjaro kwa lengo la kuwatumikisha katika mashamba ya vitunguu kwa ujira wa Sh. 1000 kwa kutwa.

Kamanda Boaz, aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni George Benard massawe( 41), mkazi wa pasua, Lameck Juma Mziray (38), mkazi wa majengo kwa mtei Moshi, Innocent Marandu (34), mkazi wa Dsm street moshi ambao wanashikiliwa na jeshi hilo kwa uchunguzi zaidi na baada ya uchunguzi kukamilika watafikishwa mahakamani.

Kamanda wa polisi alitoa wito kwa wananchi ,wazazi/walezi na jamii kwa ujumla kushirikiana na jeshi la polisi katika kulinda haki za watoto na kuwataka kuacha tabia ya kuwatumikisha watoto wadogo, pia aliongezea kuwa jeshi la polisi lipo macho kuhakikisha linapambana na kudhibiti vitendo kama hivyo.

Kwa upande mwingine, baadhi ya wananchi wa maeneo hayo, walionyesha kusikitishwa na kitendo hicho na kusema  kuwa mtu mzima hulipwa kuanzia Sh.20000 na zaidi, kwa hiyo, kitendo cha kuwatumikisha watoto wadogo kwa kuwalipa tuta Sh.1000 ni unyanyasaji mkubwa na ukiukwaji wa haki za binadamu.

Wananchi hao walilitaka jeshi la polisi mkoani hapo kuchukua hatua kali kwa watu wanaojihusisha na vitendo kama hivyo vinavyokiuka haki za watoto katika sekta mbalimbali hapa nchini.(Na Mary Mosha Moshi)



Habari Zingine

0 MAOINI :

Fadhili Athumani



EastAfrica Swahili Blogger, Journalist at Mwanaspoti Kenya, Nairobi Kenya, Call: +254705246475, whatsapp:+255654724337, Email: fadhiliathumani85@gmail.com

Proudly Powered by EAMG .